Friday, April 26, 2013

Afrika Mashariki:Tanzania tajiri wa madini, Gesi watu maskini

Nchi ya Tanzania imeshika nafasi ya pili kwa kuwa na watu maskini kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ikiongozwa na Burundi.
Utafiti uliofanywa na Benki ya Dunia (WB) na Shirika la Fedha Duniani (IMF) mwaka huu, umebaini kwamba katika nchi za Afrika Mashariki, Uganda inaongoza kwa kutokuwa na watu maskini.
Utafiti huo ulibaini Tanzania ina asilimia 67.87 ikifuatiwa na Burundi ambao wana asilimia 81.32. Ukiacha Tanzania nchi inayofuatia ni  Rwanda ambayo utafiti huo ulibaini kuwa ilikuwa na asilimia  63.17, huku  watu wa Kenya wakiwa na alama za umaskini kwa asilimia 43.37,  Uganda 38.01.
Kwa mujibu wa ripoti ya Global Monitoring ya mwaka 2013, matokeo ya utafiti huo yaliangalia idadi ya watu wanaoishi kwa Dola 1.25 sawa na Sh2,000 kwa siku.
Kwa utafiti huu, Tanzania na Burundi zinakuwa nchi zenye idadi kubwa ya watu maskini katika nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, nchi za chini ya jangwa la Sahara zinajikongoja katika kufikia malengo ya maendeleo ya milenia. Mwaka 1990 nchi za chini ya Jangwa la Sahara na Asia Mashariki zote zilikuwa na asilimia 55 wakati zilipoanza safari ya kuelekea maendeleo ya milenia.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo,  mwaka 2010 Asia Mashariki ilifanya jitihada kubwa za kupunguza umaskini hadi kufikia asilimia 12 wakati nchi za chini ya Jangwa la Sahara zilikuwa zina asilimia 48 ya umaskini.
Barani Afrika ukuaji wa miji umeongeza kutoka asilimia 30 mwaka 1980 hadi asilimia 50 mwaka 2011.
“Ukuaji wa miji unasaidia watu kuondokana na umasikini na kuelekea katika malengo ya Milenia, lakini kama hautasimamiwa vizuri unaweza kusababisha ukuaji holela wa miji, uchafuzi wa mazingira na ongezeko la uhalifu,” inasema ripoti hiyo.
Zaidi ya asilimia 80 ya bidhaa zinazozalishwa ulimwenguni zinazalishwa mijini, na kusababisha ukuaji wa miji na kupunguza umaskini. Nchi nyingi za Asia Mashariki na Marekani zimefanikiwa sana kupunguza umaskini kwa kupiti njia hii.
“Kinyume chake, Asia Kusini na nchi za chini ya Jangwa la Sahara zina idadi kubwa ya watu maskini na zinaendelea kujikongoja kuelekea katika maendeleo ya Milenia.” inabainisha sehemu ya ripoti hiyo ya WB.
Wachumi Tanzania
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe Tanzania, Dk Honest Ngowi anasema kimsingi umaskini ulioanishwa na ripoti hiyo ni umaskini wa kipato na anasema licha ya kuwa tuna raslimali nyingi kama madini, utalii na nyingine, lakini hoja inayokuja ni je zinatumiwa vipi?
“Ni sawa madini yanachimbwa, lakini wawekezaji ndiyo wengi, lakini sekta hii ya madini haina mwingiliano wa moja kwa moja na watu, na kama watu wa kawaida hawahusiki moja kwa moja inakuwa vigumu kuinuka kimapato,” anasema mhadhiri huyo.
Mtaalamu huyo wa uchumi anabainisha kwamba ili mtu awe na kipato ni lazima afanye kazi.
“Kama watu wengi hawafanyi kazi ni lazima umaskini utaendelea,” anasema.
Dk Ngowi anasema hapana budi kuwashirikisha wananchi katika soko la ajira na  masuala ya ujuzi yanachukua sehemu kubwa. Dk Ngowi anakiri kuwa mambo hayo ni changamoto kubwa kwa Taifa.
Naye Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam(UDSM) Profesa Humphrey Moshi anasema uchumi wa Tanzania ambao umeripotiwa kukua katika kipindi cha miaka 10 haupunguzi umaskini.
“Uchumi umekuwa ukiwanufaisha watu wachache, zaidi umekuwa katika miji mikubwa kama Dar es Salaam, Mwanza na Arusha,” anasema Prof. Moshi.
Profesa huyo anasema kuwa inabidi sera za uchumi zibadilishwe kwa kupunguza pengo la kiuchumi lililopo kati ya maeneo ya mijini na vijijini.
Anasema kuna hali kubwa ya matabaka  na watu  walionacho wanazidi kupata huku maskini wakizidi kuwa maskini.
Mhadhiri huyo wa UDSM anasisitiza zaidi kwamba sekta ya viwanda haina budi kuboreshwa kwa kuhakikisha kuwa inakua.
Kuhusu kilimo, Profesa Moshi anasema licha ya kuwa sekta hiyo inaajiri watu wengi, lakini haipati raslimali za kutosha.
Watanzania wanazidiwa na wenzao wa EAC licha ya nchi hii kusifika kwa kuwa na rasilimali nyingi kuliko majirani hao.
Tanzania ina ardhi kubwa inayofaa kwa kilimo na  wataalamu kadhaa wamewahi kueleza kuwa Mkoa wa Morogoro peke yake ukitumiwa vyema unaweza kuzalisha chakula na kukidhi mahitaji ya nchi nzima.
Madini kama Tanzanite ambayo yanapatikana Tanzania peke yake bado hayajawanufaisha Watanzania na inasemekana yamekuwa yakiuzwa nchi jirani badala ya soko lake kuwa nchini.
Dhahabu na almasi ni madini mengine ambayo kama yangetumiwa vyema Tanzania isingetupwa mbali na wenzake. Pia gesi ni gezo kingine cha kuwaondoa watu kwenye umaskini.
Mbali na hayo Taifa lina raslimali nyingine kama vivutio vya kitalii na mapema mwaka huu vivutio vyake vitatu Mlima Kilimanjaro, Hifadhi za Ngorongoro na Serengeti  vilishinda katika maajabu saba ya asili barani Afrika.
Katika nchi hizo tano za EAC Tanzania ndiyo yenye eneo kubwa yenye kilometa za mraba 945.0870, na pia ina idadi kubwa ya watu 44.9 milioni ambao ni raslimali kubwa zaidi ya uzalishaji na ukuzaji wa uchumi. Kenya ina watu 38.6 milioni kwa mujibu wa sensa ya 2009, na Uganda watu 32.9 milioni.
Hali inazidi kuwa ngumu zaidi kwa sababu gharama za maisha zinapanda kila siku.
Mkazi wa Tabata Kisukuru jijini Dar es Salaam, Magreth Lucas ambaye anafanya kazi ya Mamalishe anasema hali ni mbaya  kwa sababu gharama za maisha zimepanda.
“Kila kitu kimepanda, nauli juu, sokoni vitu bei juu hata biashara imekuwa ngumu wateja nao wamepungua,” anasema mama lishe huyo anayefanya biasharakatika  eneo la Tabata Relini.
Magreth anasema fedha anazopata anashindwa hata kuweka akiba kutokana na ugumu wa maisha na anafafanua kwamba analipa kodi ya nyumba Sh30,000 kwa mwezi,  nauli ya kila  siku Sh400 na chakula kila siku Sh2,000, hakuna kinachobaki
Mwananchi

0 comments:

Post a Comment